Psalms 119

Sifa Za Sheria Ya Bwana

Kujifunza Sheria Ya Bwana


1 aHeri wale walio waadilifu katika njia zao,
wanaoenenda katika sheria ya Bwana.

2 bHeri wale wanaozishika shuhuda zake,
wamtafutao kwa moyo wao wote.

3 cWasiofanya lolote lililo baya,
wanaoenenda katika njia zake.

4 dUmetoa maagizo yako
ili tuyatii kwa ukamilifu.

5 eLaiti mwenendo wangu ungekuwa imara
katika kuyatii maagizo yako!

6 fHivyo mimi sitaaibishwa
ninapozingatia amri zako zote.

7 g hNitakusifu kwa moyo mnyofu
ninapojifunza sheria zako za haki.

8 iNitayatii maagizo yako;
usiniache kabisa.

Kutii Sheria Ya Bwana


9 jKijana aifanye njia yake kuwa safi jinsi gani?
Ni kwa kutii, akilifuata neno lako.

10 kNinakutafuta kwa moyo wangu wote,
usiniache niende mbali na amri zako.

11 lNimelificha neno lako moyoni mwangu
ili nisikutende dhambi.

12 mSifa ni zako, Ee Bwana,
nifundishe maagizo yako.

13 nKwa midomo yangu nitasimulia sheria zote
zinazotoka katika kinywa chako.

14 oNinafurahia kufuata sheria zako
kama mtu afurahiaye mali nyingi.

15 pNinatafakari maagizo yako
na kuziangalia njia zako.

16 qNinafurahia maagizo yako,
wala sitalipuuza neno lako.

Furaha Katika Sheria Ya Bwana


17 rMtendee mema mtumishi wako, nami nitaishi;
nitalitii neno lako.

18 Yafungue macho yangu nipate kuona
mambo ya ajabu katika sheria yako.

19 sMimi ni mgeni duniani,
usinifiche amri zako.

20 tNafsi yangu inataabika kwa shauku kubwa
juu ya sheria zako wakati wote.

21 uUnawakemea wenye majivuno, waliolaaniwa
waendao mbali na amri zako.

22 vNiondolee dharau na dhihaka,
kwa kuwa ninazishika sheria zako.

23 Ingawa watawala huketi pamoja na kunisingizia,
mtumishi wako atatafakari juu ya maagizo yako.

24 Sheria zako ni furaha yangu,
nazo ni washauri wangu.

Kuamua Kuitii Sheria Ya Bwana


25 wNimelazwa chini mavumbini,
yahifadhi maisha yangu sawasawa na neno lako.

26 xNilikueleza njia zangu ukanijibu,
nifundishe sheria zako.

27 yNijulishe mafundisho ya mausia yako,
nami nitatafakari maajabu yako.

28 zNafsi yangu imechakazwa kwa huzuni,
uniimarishe sawasawa na neno lako.

29 aaNiepushe na njia za udanganyifu,
kwa neema unifundishe sheria zako.

30 abNimechagua njia ya kweli,
nimekaza moyo wangu katika sheria zako.

31 acNimeng’ang’ania sheria zako, Ee Bwana,
usiniache niaibishwe.

32 adNakimbilia katika njia ya maagizo yako,
kwa kuwa umeuweka moyo wangu huru.

Maombi Ili Kupata Ufahamu Wa Sheria


33 aeEe Bwana, nifundishe kuyafuata maagizo yako,
nami nitayashika mpaka mwisho.

34 afNipe ufahamu, nami nitaishika sheria yako
na kuitii kwa moyo wangu wote.

35 agNiongoze kwenye njia ya amri zako,
kwa kuwa huko napata furaha.

36 ahUgeuze moyo wangu kuelekea sheria zako,
na siyo kwenye mambo ya ubinafsi.

37 aiGeuza macho yangu kutoka kwenye mambo yasiyofaa,
uyahifadhi maisha yangu sawasawa na neno lako.

38 ajMtimizie mtumishi wako ahadi yako,
ili upate kuogopwa.

39 akNiondolee aibu ninayoiogopa,
kwa kuwa sheria zako ni njema.

40 alTazama jinsi ninavyoonea shauku mausia yako!
Hifadhi maisha yangu katika haki yako.

Kuitumainia Sheria Ya Bwana


41 amEe Bwana, upendo wako usiokoma unijie,
wokovu wako sawasawa na ahadi yako,

42 anndipo nitakapomjibu anayenidhihaki,
kwa kuwa ninalitumainia neno lako.

43 aoUsilinyakue neno la kweli kutoka kinywani mwangu,
kwa kuwa nimeweka tumaini langu katika amri zako.

44 apNitaitii amri yako daima,
naam, milele na milele.

45 aqNitatembea nikiwa huru,
kwa kuwa nimejifunza mausia yako.

46 arNitasema sheria zako mbele za wafalme
wala sitaaibishwa,

47 askwa kuwa ninazifurahia amri zako
kwa sababu ninazipenda.

48 atNinaziinulia amri zako ambazo ninazipenda mikono yangu,
nami ninatafakari juu ya maagizo yako.

Matumaini Katika Sheria Ya Bwana


49 auKumbuka neno lako kwa mtumishi wako,
kwa sababu umenipa tumaini.

50 avFaraja yangu katika mateso yangu ni hii:
Ahadi yako inahifadhi maisha yangu.

51 awWenye majivuno wamenisimanga bila kuchoka,
hata hivyo sitaiacha sheria yako.

52 axEe Bwana, ninazikumbuka sheria zako za zamani,
nazo zinanifariji.

53 ayNimeshikwa sana na ghadhabu kwa ajili ya waovu,
ambao wameacha sheria yako.

54 azMaagizo yako ni kiini cha nyimbo zangu
popote ninapoishi.

55 baEe Bwana, wakati wa usiku ninalikumbuka jina lako,
nami nitatii sheria yako.

56 bbHili limekuwa zoezi langu:
nami ninayatii mausia yako.

Kujitolea Katika Sheria Ya Bwana


57 bcEe Bwana, wewe ni fungu langu,
nimeahidi kuyatii maneno yako.

58 bdNimetafuta uso wako kwa moyo wangu wote,
nihurumie sawasawa na ahadi yako.

59 beNimezifikiri njia zangu
na nimeelekeza hatua zangu katika mausia yako.

60 bfNitafanya haraka bila kuchelewa
kuzitii amri zako.

61 bgHata waovu wanifunge kwa kamba,
sitasahau sheria yako.

62 bhUsiku wa manane ninaamka kukushukuru
kwa sababu ya sheria zako za haki.

63 biMimi ni rafiki kwa wale wote wakuchao,
kwa wote wanaofuata mausia yako.

64 bjEe Bwana, dunia imejaa upendo wako,
nifundishe maagizo yako.

Thamani Ya Sheria Ya Bwana


65 bkMtendee wema mtumishi wako
Ee Bwana, sawasawa na neno lako.

66 blNifundishe maarifa na uamuzi mzuri,
kwa kuwa ninaamini amri zako.

67 bmKabla sijapata shida nilipotea njia,
lakini sasa ninalitii neno lako.

68 bnWewe ni mwema, unalotenda ni jema,
nifundishe maagizo yako.

69 boIngawa wenye majivuno wamenisingizia uongo,
nitafuata mausia yako kwa moyo wangu wote.

70 bpMioyo yao ni katili na migumu,
bali mimi napendezwa na sheria yako.

71 bqIlikuwa vyema mimi kupata shida
ili nipate kujifunza maagizo yako.

72 brSheria inayotoka kinywani mwako ina thamani kubwa kwangu
kuliko maelfu ya vipande vya fedha na dhahabu.

Haki Ya Sheria Ya Bwana


73 bsMikono yako ilinifanya na kuniumba,
nipe ufahamu niweze kujifunza amri zako.

74 btWakuchao wafurahie wanaponiona,
kwa kuwa nimeweka tumaini langu katika neno lako.

75 buEe Bwana, ninajua kwamba sheria zako ni za haki,
katika uaminifu wako umeniadhibu.

76 bvUpendo wako usiokoma uwe faraja yangu,
sawasawa na ahadi yako kwa mtumishi wako.

77 Huruma yako na inijie ili nipate kuishi,
kwa kuwa naifurahia sheria yako.

78 bwWenye majivuno na waaibishwe kwa kunikosea mimi bila sababu,
lakini mimi nitatafakari juu ya mausia yako.

79 bxWale wakuchao na wanigeukie mimi,
hao ambao wanazielewa sheria zako.

80 byMoyo wangu usiwe na lawama katika kutii maagizo yako,
ili nisiaibishwe.

Maombi Kwa Ajili Ya Kuokolewa


81 bzNafsi yangu inazimia kwa kutamani wokovu wako,
lakini nimeweka tumaini langu katika neno lako.

82 caMacho yangu yamefifia, nikingoja ahadi yako;
ninasema, “Utanifajiri lini?”

83 cbIngawa nimekuwa kama kiriba kwenye moshi,
bado sijasahau maagizo yako.

84 Mtumishi wako itampasa angoje mpaka lini?
Ni lini utawaadhibu washtaki wangu?

85 ccWenye majivuno wananichimbia mashimo,
kinyume na sheria yako.

86 cdAmri zako zote ni za kuaminika;
unisaidie, kwa sababu watu wananishtaki bila sababu.

87 ceWalikaribia kabisa kunifuta kutoka uso wa dunia,
lakini sijaacha mausia yako.

88 cfYahifadhi maisha yangu sawasawa na upendo wako,
nami nitatii sheria za kinywa chako.

Imani Katika Sheria Ya Bwana


89 cgEe Bwana, neno lako ni la milele,
linasimama imara mbinguni.

90 chUaminifu wako unaendelea kwa vizazi vyote,
umeiumba dunia, nayo inadumu.

91 ciSheria zako zinadumu hadi leo,
kwa kuwa vitu vyote vinakutumikia.

92 cjKama nisingefurahia sheria yako,
ningeangamia katika taabu zangu.

93 ckSitasahau mausia yako kamwe,
kwa maana kwayo umehifadhi maisha yangu.

94 clUniokoe, kwa maana mimi ni wako,
kwa kuwa nimetafuta mausia yako.

95 cmWaovu wanangojea kuniangamiza,
bali mimi ninatafakari sheria zako.

96 cnKatika ukamilifu wote ninaona mna kikomo,
lakini amri zako hazina mpaka.

Kuipenda Sheria Ya Bwana


97 coAha! Tazama, sheria yako naipenda mno ajabu.
Ninaitafakari mchana kutwa.

98 cpAmri zako zimenipa hekima zaidi kuliko adui zangu,
kwa kuwa nimezishika daima.

99 cqNina akili zaidi kuliko walimu wangu wote,
kwa kuwa ninatafakari juu ya sheria zako.

100 crNina ufahamu zaidi kuliko wazee,
kwa kuwa ninayatii mausia yako.

101 csNimezuia miguu yangu isiende kwenye kila njia mbaya,
ili niweze kutii neno lako.

102 ctSijaziacha sheria zako,
kwa kuwa umenifundisha wewe mwenyewe.

103 cuTazama jinsi maneno yako yalivyo matamu kwangu,
matamu kuliko asali katika kinywa changu!

104 cvNinapata ufahamu kutoka mausia yako,
kwa hiyo ninachukia kila njia ya upotovu.

Nuru Kutoka Kwenye Sheria Ya Bwana


105 cwNeno lako ni taa ya miguu yangu
na mwanga katika njia yangu.

106 cxNimeapa na nimethibitisha,
kwamba nitafuata sheria zako za haki.

107 cyNimeteseka sana, uhifadhi maisha yangu, Ee Bwana,
sawasawa na neno lako.

108 czEe Bwana, pokea sifa za hiari za kinywa changu,
nifundishe sheria zako.

109 daIngawa maisha yangu yako hatarini siku zote,
sitasahau sheria yako.

110 dbWaovu wamenitegea mtego,
lakini sijayakiuka maagizo yako.

111 dcSheria zako ni urithi wangu milele,
naam ni furaha ya moyo wangu.

112 ddNimekusudia moyoni mwangu
kuyafuata maagizo yako mpaka mwisho.

Usalama Ndani Ya Sheria Ya Bwana


113 deNinachukia watu wa nia mbili,
lakini ninapenda sheria yako.

114 dfWewe ni kimbilio langu na ngao yangu,
nimeweka tumaini langu katika neno lako.

115 dgOndokeni kwangu, ninyi mtendao mabaya,
ili niweze kushika amri za Mungu wangu!

116 dhNihifadhi sawasawa na ahadi yako, nami nitaishi;
usiache matumaini yangu yakavunjwa.

117 diNitegemeze, nami nitaokolewa,
nami daima nitayaheshimu maagizo yako.

118 djUnawakataa wote wanaoyaasi maagizo yako,
kwa maana udanganyifu wao ni bure.

119 dkWaovu wa nchi unawatupa kama takataka,
kwa hivyo nazipenda sheria zako.

120 dlMwili wangu unatetemeka kwa kukuogopa wewe,
ninaziogopa sheria zako.

Kuitii Sheria Ya Bwana


121 dmNimetenda yaliyo haki na sawa,
usiniache mikononi mwa watesi wangu.

122 dnMhakikishie mtumishi wako usalama,
usiache wenye kiburi wanionee.

123 doMacho yangu yamefifia, yakitazamia wokovu wako,
na kuitazamia ahadi yako ya kweli.

124 dpMfanyie mtumishi wako kulingana na upendo wako
na unifundishe maagizo yako.

125 dqMimi ni mtumishi wako; nipe ufahamu
ili niweze kuelewa sheria zako.

126 drEe Bwana, wakati wako wa kutenda umewadia,
kwa kuwa sheria yako inavunjwa.

127 dsKwa sababu nazipenda amri zako zaidi ya dhahabu,
naam, zaidi ya dhahabu safi,

128 dtna kwa sababu naona maagizo yako yote ni adili,
nachukia kila njia potovu.

Shauku Ya Kuitii Sheria Ya Bwana


129 duSheria zako ni za ajabu,
hivyo ninazitii.

130 dvKuingia kwa maneno yako kunaleta nuru,
kunampa mjinga ufahamu.

131 dwNimefungua kinywa changu na kuhema,
nikitamani amri zako.

132 dxNigeukie na unihurumie, kama uwafanyiavyo siku zote
wale wanaolipenda jina lako.

133 dyOngoza hatua zangu kulingana na neno lako,
usiache dhambi yoyote initawale.

134 dzNiokoe na uonevu wa wanadamu,
ili niweze kutii mausia yako.

135 eaMwangazie mtumishi wako uso wako
na unifundishe amri zako.

136 ebChemchemi za machozi zinatiririka kutoka machoni yangu,
kwa kuwa sheria yako haifuatwi.

Haki Ya Sheria Ya Bwana


137 ecEe Bwana, wewe ni mwenye haki,
sheria zako ni sahihi.

138 edSheria ulizoziweka ni za haki,
ni za kuaminika kikamilifu.

139 eeJitihada yangu imenidhoofisha, kwa kuwa adui zangu
wanayapuuza maneno yako.

140 efAhadi zako zimejaribiwa kikamilifu,
mtumishi wako anazipenda.

141 egIngawa ni mdogo na ninadharauliwa,
sisahau mausia yako.

142 ehHaki yako ni ya milele,
na sheria yako ni kweli.

143 eiShida na dhiki zimenipata,
lakini amri zako ni furaha yangu.

144 ejSheria zako ni sahihi milele,
hunipa ufahamu ili nipate kuishi.

Maombi Kwa Ajili Ya Kuokolewa


145 ekEe Bwana, ninakuita kwa moyo wangu wote,
nami nitayatii maagizo yako.

146 elNinakuita; niokoe
nami nitazishika sheria zako.

147 emNinaamka asubuhi na mapema na kukuomba msaada;
nimeweka tumaini langu katika neno lako.

148 enSikufumba macho yangu usiku kucha,
ili niweze kutafakari juu ya ahadi zako.

149 eoUsikie sauti yangu sawasawa na upendo wako,
Ee Bwana, uyahifadhi maisha yangu, sawasawa na sheria zako.

150 epWale wanaopanga mipango miovu wako karibu nami,
lakini wako mbali na sheria yako.

151 eqEe Bwana, hata hivyo wewe u karibu,
na amri zako zote ni za kweli.

152 erTangu zamani nimejifunza kutoka shuhuda zako
kwamba umezithibitisha ili zidumu milele.

Maombi Kwa Ajili Ya Msaada


153 esYaangalie mateso yangu, uniokoe,
kwa kuwa sijasahau sheria yako.

154 etNitetee katika hali hii yangu na unikomboe,
uyahifadhi maisha yangu sawasawa na ahadi yako.

155 euWokovu uko mbali na waovu,
kwa kuwa hawatafuti maagizo yako.

156 evEe Bwana, huruma zako ni kuu,
uyahifadhi maisha yangu sawasawa na sheria zako.

157 ewAdui wanaonitesa ni wengi,
lakini mimi sitaziacha sheria zako.

158 exNinawatazama wasioamini kwa chuki,
kwa kuwa hawalitii neno lako.

159 eyTazama jinsi ninavyopenda mausia yako;
Ee Bwana, uyahifadhi maisha yangu, sawasawa na upendo wako.

160 ezManeno yako yote ni kweli,
sheria zako zote za haki ni za milele.

Kujiweka Wakfu Kwa Sheria Ya Bwana


161 faWatawala wamenitesa bila sababu,
lakini moyo wangu unatetemeka kwa neno lako.

162 fbNafurahia ahadi zako
kama mtu aliyepata mateka mengi.

163 Ninachukia na kuchukizwa sana na uongo,
lakini napenda sheria yako.

164 fcNinakusifu mara saba kwa siku,
kwa ajili ya sheria zako za haki.

165 fdWanaopenda sheria yako wana amani tele,
wala hakuna kitu kinachoweza kuwakwaza.

166 feEe Bwana, ninangojea wokovu wako,
nami ninafuata amri zako,

167 ffNinazitii sheria zako,
kwa sababu ninazipenda mno.

168 fgNimetii mausia yako na sheria zako,
kwa kuwa njia zangu zote zinajulikana kwako.

Kuomba Msaada


169 fhEe Bwana, kilio changu na kifike mbele zako,
nipe ufahamu sawasawa na neno lako.

170 fiMaombi yangu na yafike mbele zako,
niokoe sawasawa na ahadi yako.

171 fjMidomo yangu na ibubujike sifa,
kwa kuwa unanifundisha maagizo yako.

172 fkUlimi wangu na uimbe kuhusu neno lako,
kwa kuwa amri zako zote ni za haki.

173 flMkono wako uwe tayari kunisaidia,
kwa kuwa nimechagua mausia yako.

174 fmEe Bwana, ninatamani wokovu wako,
na sheria yako ni furaha yangu.

175 fnNijalie kuishi ili nipate kukusifu,
na sheria zako zinitegemeze.

176 foNimetangatanga kama kondoo aliyepotea.
Mtafute mtumishi wako,
kwa kuwa sijasahau amri zako.
Copyright information for SwhKC